Tamko la ACT-Wazalendo dhidi ya Rais Magufuli

kiongozi wa chama - Act wazalendo Ndg Zitto Kabwe
Chama cha *ACT Wazalendo* kimeshtushwa na kauli (amri) ya Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ndugu John Pombe Magufuli aliyoitoa
hivi karibuni akiwa Mkoani Tanga ya kutaka Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo
ya Mazingara, Kata ya Mkata, Wilayani Handeni , katika Mkoa wa Tanga
ahamishwe katika kituo hicho mara moja,hakimu huyo liyefahamika kwa
jina la Laizer ametakiwa kuhamishwa katika kituo hicho, kufuatia kutuhumiwa
kupendelea wafugaji katika kesi za Wakulima dhidi ya Wafugaji.
Rais Magufuli alitoa kauli hiyo baada
ya kupokea malalamiko ya Mkuu wa Wilaya ya Korogwe, Godwin Gondwe dhidi
ya Hakimu huyo akimtuhumu kuwa kesi zote kati ya wakulima na wafugaji
katika mahakama hiyo, wanaoshinda katika kesi hizo ni wafugaji, na
kwamba anapendelea wafugaji.
Kupitia taarifa kwa vyombo vya habari
iliyotolewa leo Agosti 9, 2017 na Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria na
Katiba ACT, Thomas Msasa, amesema chama hicho kinalaani kauli hiyo, kwa
madai kuwa inakiuka misingi ya Katiba ya nchi inayoipa Mahakama haki na
uhuru wa kufanya kazi yake bila kuingiliwa na mihimili mingine.
“Kauli hii inakiuka Katiba ya nchi
ya mwaka 1977, Ibara 107b ambayo inaipa mahakama haki na uhuru wa
kufanya kazi yake bila ya kuingiliwa wala kubughudhiwa na mihimili
mingine. Katiba inaainisha mgawanyo wa madaraka baina ya Serikali,
Mahakama na Bunge,” amesema na kuongeza.
“Kitendo cha Ndugu Rais kutaka
Hakimu wa Mahakama achukuliwe hatua kwa kuhamishwa ni kuingilia mhimili
wa mahakama. Tunaamini kuwa hata kama tuhuma dhidi ya hakimu mhusika ni
za kweli, basi lazima utaratibu wa hatua za kinidhamu kwa hakimu huyo
zifuatwe kwa kuchunguzwa kwanza, kupata ushahidi na akikutwa na hatia
achukuliwe hatua na mamlaka yake ya nidhamu ambayo ni Tume ya Utumishi
wa Mahakama.”
Aidha, Msasa amevitaka vyama vya
mawakili vya Tanganyika na Zanzanzibar na taasisi nyingine kupigania
utawala wa Katiba na Sheria nchini kwa kuilaani kauli hiyo. Pia amesema
ACT inamsihi Rais Magufuli kumchukulia hatua za kiutawala Gondwe kwa
madai kuwa amemuingiza kwenye mgogoro wa Kikatiba usio wa lazima.
Post a Comment: