TAARIFA KWA UMMA KUHUSU KUIMARISHA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YA BARAZA LA TAIFA LA HIFADHI NA USIMAMIZI WA MAZINGIRA-NEMC
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA
MAKAMU WA RAIS
TAARIFA
KWA UMMA KUHUSU KUIMARISHA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YA BARAZA LA TAIFA LA
HIFADHI NA USIMAMIZI WA MAZINGIRA-NEMC
Katika
kikao kilichoitishwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na
Mazingira Mhe. January Makamba (Mb), tarehe 24 Januari 2016, mjini Dodoma
kuhusu kuimarisha utendaji ndani ya Baraza la Taifa la Hifadhi na
Usimamizi wa Mazingira-NEMC maamuzi yaliyofikiwa ni kama ifuatavyo:
1.
Kuhusu suala la kiwanda cha kusindika minofu ya punda Mkoani Dodoma,
imegundulika kulikuwa na ukiukwaji mkubwa, wa makusudi na wa wazi wa
miiko ya kazi kwa watumishi wa NEMC walioshughulika na
kiwanda hicho. Hivyo, Mhe. Makamba ameagiza watumishi wa NEMC wafuatao
wasimamishwe kazi mara moja:
a. Dkt. Eladius Makene -Afisa
Mazingira Mwandamizi,
b. Wakili Heche Suguta
Manchare - Mwanasheria Daraja la II
c. Mhandisi Boniface
Benedict Kyaruzi, Afisa Mazingira
Hatua
nyingine za kinidhamu na kisheria zitafuatia.
2.
Vilevile, imebainika kwamba usimamizi wa watumishi wa NEMC siyo makini na
thabiti na kusababisha malalamiko mengi kuhusu utendaji wa Baraza. Hivyo,
Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Mhandisi Bonaventura Baya apewe barua ya onyo kali la
mwisho kwa udhaifu katika usimamizi wa watumishi wa Baraza.
3.
NEMC kama chombo muhimu nchini kilichopewa jukumu la kusimamia utekelezaji wa
Sheria ya Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira inatarajiwa kazi zake
zifanyike kwa ufanisi wa kiwango cha juu kulingana na majukumu yaliyoko kwa
mujibu wa Sheria. Hivyo, kwa mapungufu yanayojitokeza Mhe. Makamba,
ndani ya wiki moja ataunda jopo la wataalamu wasiozidi watano ili kutathmini
utendaji wa NEMC na changamoto mbali mbali katika usimamizi wa hifadhi ya
mazingira na kuishauri Serikali ipasavyo.
4.
Ili kuimarisha ufanisi na udhibiti wa utendaji wa NEMC, ndani ya wiki
moja litatolewa Tangazo litakalokuwa na mambo yafuatayo: Anwani ya barua
pepe (email), Nukushi (fax), Namba ya simu, Namba ya Whatsapp ili mtu yeyote
mwenye malalamiko au aliyewahi kuombwa rushwa ama chochote na watumishi wa NEMC
ambacho ni kinyume na maadili ya kazi yao atoe taarifa mara moja ili
uchunguzi ufanyike na hatua zichukuliwe.
5.
Kutokana na mapungufu yanayojitokeza katika utekelezaji wa Tathmini ya Athari
kwa Mazingira, ndani ya wiki moja, NEMC ipitie upya orodha ya
wataalamu na taasisi elekezi zilizosajiliwa na kufuta wataalamu na taasisi zote
ambazo zimekuwa zikikiuka maadili ya kazi zao likiwemo suala la kuwasilisha
taarifa zilizo chini ya viwango, kuchelewesha kazi za wateja wao na
kutowasiliana na wateja wao kuhusu hatua za utekelezaji wa maombi yao.
6.
Ndani ya wiki tatu uitishwe mkutano wa dharura wa Bodi ya NEMC kujadili na
kufanya maamuzi juu ya changamoto za utendaji katika Baraza.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA MAKAMU WA RAIS
08.01.2016

Post a Comment: