Suala la kusimama mita 200 linahitaji busara
Serikali, Tume ya Taifa ya Uchaguzi na vyama vya siasa, hasa vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) viko kwenye mzozo mkubwa wa wapi wananchi wanatakiwa wasimame baada ya kupiga kura Oktoba 25.
Sura
ya 343 ya Sheria ya Uchaguzi, kifungu cha 104 (1) kinaeleza bayana kuwa
mikutano wala watu waliovalia sare za chama au mabango yenye mwelekeo wa
itikadi ya chama fulani hayataruhusiwa ndani ya eneo la mita 200 kuzunguka
kituo cha kupigia kura.
Tume
ya Uchaguzi, kwa kutumia sheria hiyo, inasisitiza watu kuwa mbali na kutotakiwa
kufanya mikutano ndani ya eneo hilo, wananchi wanatakiwa warudi nyumbani baada
ya kupiga kura siku hiyo.
Serikali
nayo inaeleza kuwa ni marufuku kwa mtu kubakia eneo la kituo kulinda kura kama
NEC inavyosisitiza kwenye matangazo yake, lakini vyama vya upinzani vinapingana
na maelezo hayo.
Chadema,
ambayo inaungwa mkono na vyama vya CUF, NLD na NCCR Mageuzi, imekuwa
ikiwasisitizia wafuasi wake kuwa watakapomaliza kupiga kura wahesabu mita 200
kutoka kituoni na hapo ndipo wasimame kulinda kura zao.
Suala
hili limezua utata mkubwa na tayari limepelekwa mahakamani kutaka tafsiri ya
sheria hiyo, hasara kipengele hicho ambacho kisipotafsiriwa vizuri, kinaweza
kuwa chanzo cha vurugu kubwa siku ya uchaguzi.
Ni
kutokana na sababu hiyo tumeona tuwasihi wahusika wote kuliangalia suala hilo
kwa makini badala ya kila upande kushikilia msimamo wake bila ya kujali athari.
Tatizo
la sheria hiyo ni kukosa uhalisia katika mazingira ya makazi ya watu. Ni kwa
nadra sana vituo vya kupigia kura vitakuwa maeneo ambayo yako mbali na makazi
ya wananchi. Vingi viko ndani ya uzio wa mita zisizozidi 50 na hivyo wakati
wowote polisi, ambao wanasimamia utekelezwaji wa sheria, wanaweza kuwakamata
watu wakati wowote ule kwa kosa la kufanya mkutano ndani ya mita 200 bila ya
kujali kuwa eneo walilokamatwa ni makazi yao.
Polisi
wanaweza kutafsiri uvunjwaji wa sheria hiyo hata pale wanafamilia watakapokuwa
kwenye shughuli zao za kijamii siku hiyo na hivyo kuamsha vurugu ambazo
zinaweza kuepukika iwapo busara itatumika.
Serikali,
NEC, Jeshi la Polisi na vyama vya siasa hawana budi kuacha kutoa kauli kali
zinazoonyesha kutobadilika kwa misimamo yao na badala yake wakutane na
kutathmini njia bora ya kuhakikisha sheria hiyo inaheshimiwa na wakati huohuo,
amani inalindwa.
Siku
zote pande zinazovutana zinapokutana, hupatikana njia bora ya kumaliza tatizo
kuliko kila upande kutangaza misimamo yake kwa wakati wake na kuendelea
kuchanganya wananchi.
Misimamo
kama hiyo inawaandaa wananchi kwa vurugu, inawatisha wananchi kwenda kupiga
kura kwa kuhofia vurugu zinaweza kutokea wakati wowote na inajenga picha kuwa
wizi ni lazima utokee. Hakuna wakati ambao uchaguzi umetawaliwa na amani kama
mwaka huu. Kumekuwa na matukio machache ya kuvunjika kwa amani tofauti na miaka
mingine na pia Jeshi la Polisi limetekeleza wajibu wake sehemu nyingi bila ya
kutumia nguvu za ziada kulinganisha na chaguzi zilizopita.
Ni
rai yetu kuwa mwenendo huu usitibuliwe hatua za mwisho za uchaguzi kwa sababu
tu ya utekelezaji wa kipengele hicho.
Tuna
imani kuwa pande zinazohusika zitakutana mapema iwezekanavyo kujadili suala
hilo na kulipatia suluhisho litakalokubaliwa na wote ili Uchaguzi Mkuu uishe
kwa amani.
Post a Comment: